0
UWEZEKANO wa kufanyika kwa Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, umeanza kupungua na kusababisha Kamati Kuu (CCM) ya Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM, kuagiza Serikali na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kutafakari upya kura hiyo.
Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu kikao cha CC ya chama hicho kilichofanyika kuanzia juzi asubuhi mpaka zaidi ya saa sita za usiku.
Kwa mujibu wa Nape, CC ilipokea taarifa kuhusu mwenendo wa Kura ya Maoni na baada ya kuitafakari kwa kina na kwa kuzingatia changamoto zilizopo ikiwemo ya Uchaguzi Mkuu mwaka huu, wameona watoe ushauri huo.

Akielezea changamoto walizoziona, Nape alisema wamebaini moja ni kasi ndogo ya uboreshwaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura, ambalo hata NEC imeshasema kuwa, Kura ya Maoni haitafanyika bila kukamilika kwa daftari hilo.

Changamoto ya pili ameielezea kuwa ni matakwa ya kisheria, ambayo ni kuwa na siku 60 za kutoa elimu ya Katiba Inayopendekezwa na siku 30 za kampeni, ambapo inaonekana wanaweza kujikuta wamefikia Uchaguzi Mkuu kabla kura hiyo haijafanyika.

"Tunadhani ni wakati muhimu Serikali ikae na NEC ambao ni wadau kisheria wa suala hili, kujadiliana kuona wanaliwekaje suala hili, kama ni kuhitimisha au watafanyaje lakini kwa kuzingatia maslahi mapana ya Taifa letu," alisema Nape.

Akifafanua zaidi alisema pia ipo changamoto ya Uchaguzi Mkuu wenyewe, ambao Taifa linaukaribia ambao Kikatiba ni Jumapili ya mwisho ya Oktoba, itakayokuwa tarehe 25.
Nape alisema baada ya kuhesabu siku zilizobakia kabla ya kufikia siku ya Uchaguzi Mkuu, wamebaini kutakuwa na changamoto ambazo wameona zinatakiwa kufanyiwa kazi, ili kutoa muda kwa Uchaguzi Mkuu ufanyike kwanza bila kuingiliwa na mambo mengine.

Akizungumzia uwezekano wa kufanya uchaguzi pamoja na Kura ya Maoni, Nape alisema sheria haizuii lakini aliwahi kuhudhuria kikao kimoja cha Tume, baada ya mjadala walikubaliana kuwa suala hilo haliwezekani.

Alifafanua kuwa hawawezi kuruhusu Katiba ivunjwe kwa kushindwa kufanya uchaguzi kwa muda unaopangwa kutokana na Kura ya Maoni.(HABARI LEO)

Chapisha Maoni

 
Top